LOWASSA NJE URAIS CCM, MAKAMBA, MAGUFULI, MEMBE KUCHUANA NA MIGIRO NA AMINA SALUM

Na Mwandishi Wetu, DODOMA
CHAMA cha Mapinduzi (CCM) imetaja majina matano ya waomba kugombea Urais kwa tiketi ya chama chake walioingia hatua ya pili, ambao ni Bernard Membe, John Magufuli, January Makamba, Asha Rose Migiro na Amina Salum Ali.
Baada ya kikao hicho saa saba kasoro kidogo usiku wa jana, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alikataa kutaja majina yaliyopitishwa, lakini akaunti ya Twitter ya CCM, ikawataja waliopitishwa kuwa ni Bernard Membe, Dk John Magufuli, Dk Asha Rose Migiro, January Makamba na Amina Salum Ali na kuwatupa wengine 33 akiwamo Edward Lowassa.
“Kikao cha Kamati Kuu kimeisha salama. Kesho (leo) Halmashauri Kuu itakutana kuanzia saa 4:00 asubuhi,” alisema Nape baada ya kikao hicho.
Alipotakiwa kutaja majina ya makada watano waliopitishwa, Nape alisema: “Nimeambiwa mchakato bado unaendelea na kesho (leo) Halmashauri Kuu itakutana kuendelea na kazi. Kwa hiyo nawakaribisha kesho kuanzia saa 4:00 asubuhi mje mchukue picha, habari, karibu sana.” Mkutano Mkuu utafanyika saa nane mchana leo.”
Dakika chache baada ya kikao hicho kumalizika, wajumbe watatu wa Kamati Kuu, wakiongozwa na mbunge wa Songea Mjini, Dk Emmanuel Nchimbi waliitisha mkutano na waandishi wa habari na kueleza kuwa wanapinga uamuzi huo ambao hawakuutaja, wakidai kuwa si majina yote yaliyowasilishwa mbele ya kamati hiyo.
Dk Nchimbi, akiongozana na mwenyekiti wa CCM wa Mkoa wa Dodoma, Adam Kimbisa na mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT), Sofia Simba waliwaeleza waandishi wa habari mara tu baada ya mkutano wa Kamati Kuu kuwa kikao hicho hakikufuata kanuni kwa kuwa majina machache yaliwasilishwa na hayakuhusisha mgombea anayekubalika.
Ingawa hawakumtaja mgombea huyo waliyesema anatajwa na wengi, wajumbe hao wanafahamika kuwa wanamuunga mkono Lowassa.
Baada ya kikao hicho taarifa za wagombea hao zilisambaa kwa kasi katika mitandao ya kijamii na mijadala ya wazi ilianza kuhusu uamuzi wa kumtosa Lowassa, ambaye alikuwa Waziri Mkuu wa kwanza wa Serikali ya Awamu ya Nne.
Mmoja wa makada watano waliopitishwa kwenye mchujo huo aliithibitishia Mwananchi kuwa jina lake limepita, lakini akasema hataki akaririwe na badala yake akamshauri mwandishi aangalie akaunti ya twitter ya CCM baada ya nusu saa.
Habari za jina la Lowassa kukatwa zilizagaa tangu jana asubuhi, ilipoelezwa kuwa CCM ilifanya majadiliano na wadau mbalimbali kuangalia jinsi ya kudhibiti watu wanaounga mkono baada ya kupata taarifa kuwa ameenguliwa.
Share on Google Plus

About Mahmoud Bin Zubeiry

Mahmoud Zubeiry Works at BIN ZUBEIRY "BIN ZUBEIRY" Tangaza nasi hapa.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment